Wednesday, October 24, 2012

Kwa nini Kadinali Rugambwa kazikwa mara mbili?


 Msafara kwa ajili ya mazishi ya Kadinali Rugambwa Oktoba 6 mwaka huu.
Oktoba 6, 2012, siku ya Jumamosi, mwili wa marehemu Laurian Kadinali Rugambwa, ulihamishwa kutoka kwenye kanisa la Kashozi Bukoba, alikozikwa kwa muda na kuzikwa rasmi kwenye kanisa la Jimbo Katoliki la Bukoba. 

Mwili huo ulizikwa Kashozi kwa muda mnamo mwaka 1997, kwa vile kanisa kuu la jimbo la Bukoba lilikuwa linafanyiwa ukarabati mkubwa.

 Jeneza lenye mwili wa Kadinali Rugambwa
Parokia ya Kashozi, iko umbali wa kama kilomita 25 kutoka Bukoba mjini ukielekea upande wa Sekondari ya Ihungo na Nyakato. Kanisa la Kashozi ni la kwanza kujengwa jimbo la Bukoba.


Wakati wa mazishi ya muda yaliyofanyika mwaka wa 1997, Askofu wa Jimbo Katoliki la Bukoba, Mhashamu Askofu Nestory Timanywa, aliwaambia waumini na wote walioshiriki mazishi hayo kwamba mwili wa Kadinali Rugambwa, utatunzwa hapo Kashozi kwa muda wa miaka miwili, hadi hapo kanisa litakapokamilika.


 Wananchi wamejipanga barabarani kushuhudia jeneza lenye mwili wa Kadinali wa kwanza Mwafrika, Laurean Rugambwa, Oktoba 6 mwaka huu.
Mwadhama Polycarp Kadinali Pengo kwenye mazishi ya muda, aliwaambia watu wa Bukoba kwamba siku ya mazishi rasmi ikifika, wasipomjulisha ili aje kumzika Rugambwa, atawashitaki! Wakati huo alikuwa hajatangazwa kuwa Kadinali, lakini aliongea kwa kujiamini kwamba yeye ndiye mrithi wa Kadinali Rugambwa.

Taarifa zinatujulisha kwamba Kadinali Pengo hataweza kumzika Rugambwa kwa vile yuko Roma, kwa kazi maalumu. Mungu, bariki hatawashitaki watu wa Bukoba, maana taarifa ya mazishi ameipata, ila ameshindwa kufika.

Gari lililobeba mwili wa Kadinali Rugambwa Oktoba 6 ,2012.
Mazishi haya ya pili yanawachanganya wengi. Wanajiuliza maana yake ni nini? Ni kwamba kabla ya kifo cha Kadinali Rugambwa, aliomba “Kwa unyenyekevu” kwamba akifa, azikwe Bukoba kwenye kanisa alilolijenga yeye na kulitolea kwa ‘Mama. Hayo ndo yalikuwa mapenzi yake. Na kawaida wosia wa mtu unaheshimiwa. Kuna watu wachache wasiokuwa na busara wanaopuuzia wosia. 

Kadinali Pengo, aliheshimu wosia wa Kadinali Rugambwa wa kuzikwa Bukoba, ndio maana hakuzikwa Dar-es-Salaam, jimbo aliloliongoza hadi anastaafu.
Kadinali Pengo, alifafanua zaidi juu ya Kadinali Rugambwa kuzikwa Bukoba: 
“… kuna watu wanataka wamfahamu Kadinali Rugambwa, zaidi alivyojifahamu yeye mwenyewe. Yeye alijua kwamba kuzikwa Dar-es-Salaam, hakuihitaji kuomba ruhusa, lakini kuzikwa Bukoba, alihitaji kuomba ruhusa.



Akachagua la pili la kuomba ruhusa… akachagua kuzikwa huku maporini…Alijua ni mtu muhimu kwenye kanisa na watu wangependa kutembelea kaburi lake… ingekuwa rahisi kama angezikwa Dar-es-Salaam, lakini yeye alichagua huku. Tuheshimu uamuzi wake. Uvumi kwamba nimekataa kumzika Dar-es-Salaam si kweli, kama niliweza kuishi naye akiwa hai, ningeshindwa kuishi naye akiwa kaburini?”

 Mwadhama Laurian Kadinali Rugambwa, alikuwa mtu wa kimataifa. Kwa nafasi yake ndani ya kanisa angeweza kuzikwa hata Roma, maana kila Kadinali ana kanisa lake kule Roma.

Hivyo angeweza hata kuzikwa Dar-es- Dalaam. Lakini kumbe ndani kabisa ya moyo wake, bado alitamani azikwe nyumbani kwao.

 Kaburi la Kadinali Rugambwa
Kuna mambo mengi ya kuandika juu ya Lauriani Kadinali Rugambwa, kuanzia yeye kuwa Kadinali wa kwanza mwafrika, kushughulikia elimu kwa kujenga shule, kushughulikia afya kwa kujenga hospitali, kushughulikia miito ya upadri na utawa kwa kujenga seminari na kuanzisha mashirika ya kitawa na mengine mengi.

Tatizo kubwa juu ya Kadinali Rugambwa ni kwamba hakuandika vitabu. Hivyo ni vigumu kuelezea kwa nukuu yale aliyoyaamini na kuyasimamia.

Maelezo kwa hisani ya Tanzania Daima

No comments:

Post a Comment