Mkuu
wa Jeshi la Polisi Tanzania IGP Said Mwema, akizungumza katika Mkutano
huo uliofanyika Makao Makuu ya Polisi Zanzibar Kilimani
WAKATI Serikali ya Umoja wa Kitaifa Zanzibar ikikiri kuwepo kwa watu
wanaotumia mgongo wa dini kutimiza malengo yao ya kisiasa, hali ya
hatari imezidi kugubika mji wa Zanzibar, baada ya watu wasiojulikana,
lakini wakiaminika kuwa wafuasi wa kundi la kidini la Uamsho
kuyashambulia na kuteketeza makanisa sita hadi kufikia jana.
Kadhalika, shule nyingi za msingi na sekondari, tangu juzi zimefungwa,
baadhi yake zikiwemo za bweni, huku kukiwa na habari kuwa wanafunzi
katika shule mbili walilazimishwa kurejea makwao hadi hapo hali ya
utulivu itakaporejea.
Mmoja wa wakuu wa shule hizo, ambaye aliomba jina lake na shule
vihifadhiwe, alikiri kuwa shule yake imesimamisha masomo kwa muda
usiojulikana, na kwamba wamewaruhusu wanafunzi wanaoshi bwenini kurejea
makwao.
Uchunguzi umebaini kuwa, karibu shule zote za msingi na sekondari
zinazomilikiwa na serikali na taasisi za dini, zilizoko Mjini Magharibi,
tangu juzi hazijafunguliwa, na wanafunzi wachache waliopata ujasiri wa
kufika shuleni, walirudishwa majumbani na walimu.
Hadi kufikia jana, makanisa yaliyothibitika kuchomwa moto na watu hao
wanaoaminika kuwa wafuasi wa kikundi hicho cha Uamsho ni Kanisa la EAGT,
Elimu Pentekoste, TAG, Anglikana, Katoliki na FPCT.
Askofu wa Jimbo la Zanzibar wa Makanisa ya Tanzania Assemblies of God
(TAG), Dickson Kagenga aliilaumu serikali akisema imechelewa kuchukua
hatua kukomesha vitendo vya uchomaji moto makanisa mara tu vilipoanza.
Askofu Kagenga alisema, uchomaji moto wa makanisa hayo, usingefikia
hatua hii mbaya, kama vyombo vya dola vingewakamata na kuwashughulikia
kisheria wahusika, lakini hapakuwa na hatua iliyochukuliwa, hivyo kuwapa
mwanya na jeuri watu hao kufanya wapendavyo.
Hivyo, ameiomba serikali ichukue hatua za kisheria kwa wahusika wote kwani matokeo hayo yanahatarisha maisha ya watu.
Akizungumzia suala hilo mbele ya waandishi wa habari jana, Askofu Mkuu
wa TAG, Dk. Barnabas Mtokambali, pamoja na kulaani mashambulizi hayo,
alisikitishwa na ukimya wa serikali wa muda mrefu juu ya vitendo vya
uchochezi na uvunjifu wa amani uliokuwa ukifanywa na baadhi ya viongozi
wa makundi ya kiislamu dhidi ya watu wa dini nyingine.
Alisema katika siku za hivi karibuni kumeibuka makundi ya kidini
yaliyoanza kutoa matamko yenye kuchochea ghasia za kidini, na kulitaja
kundi la JUAKATA lililowahi kufanya kongamano katika Ukumbi wa Diamond
Jubilee, jijini Dar es Salaam, kama moja ya makundi ambayo kauli zake
zinahatarisha amani.
Mtokambali alidai kuwa, katika kongamano hilo, badala ya kujadili
mambo ya dini na kudumisha amani, walihamasisha washiriki kuhakikisha
kuwa rais ajaye lazima atoke Zanzibar.
Aliongeza kuwa, mambo mengine yalikuwa haja ya kukabiliana na ukuaji
wa wakazi wa Kikristo, kupinga muungano ili kuupa nguvu Uislamu na
kupigana kufa na kupona kutetea maslahi yao katika kipindi cha kuandaa
katiba.
Askofu huyo alisema ameingiwa hofu kwa kuwa roho ya ubaguzi wa kidini
ambayo ilikemewa na Hayati Mwalimu Nyerere na kuifananisha na dhambi ya
kula nyama ya mtu imekua ikiyatafuna mataifa ya Afrika.
Alisema taswira hiyo ni mbaya, na kama haitapatiwa dawa italigawa
taifa na kulifanya kama ilivyokuwa kwa Nigeria na kwingineko barani
Afrika.
Hata hivyo, alitoa ushauri kwa serikali na viongozi wa dini kukumbuka
kuwa wana wajibu mkubwa katika jamii, hivyo ni vema wakawa makini katika
kutoa matamshi na maelekezo yao ili yasiwe chanzo cha kuchochea vurugu
za kidini na uvunjaji wa amani.
Mtokambali alisema ni vyema kwa wakati huu wa kuandikwa kwa katiba
mpya kila kikundi kikafuata utaratibu uliowekwa badala ya kuchochea
kwani madhara yake yatawakumba Watanzania wote ikiwa ni pamoja na
watoto.
“Ni vyema ieleweke kuwa matukio kama haya ya uvunjaji wa amani
yasipodhibitiwa na kukomeshwa haraka, yanaweza kuumba chuki ambayo
inaweza kuibua mlipuko mkubwa na machungu kwa wananchi na matokeo yake
yakawa mabaya kwa taifa zima,” alisema.
Waziri katika ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais, Mohammd Aboud amekiri
kuwa vurugu hizo zina mkono wa siasa ndani yake, na kwamba serikali
ilikosea kudhani kuwa wahusika ni viongozi wa dini.
Akiwa katika ziara yake kukagua uharibifu uliofanywa katika Kanisa la
Kariakoo, Waziri Aboud alisema serikali imekosea kuwaachia watu ambao
wametumia kivuli cha dini kutekeleza matakwa yao ya kisiasa wakati
taasisi zao zimesajiliwa rasmi kidini.
Kutokana na kubainika kwa jambo hilo, serikali imeamua kuendesha msako
mkali kuwakamata watu wote watakaohubiri maneno yatakayohamasisha
vurugu.
Alisema serikali iko wazi kusikiliza maoni ya mwananchi yeyote
yatakayofuata utaratibu, sheria na kanuni za nchi kwa nia ya kujenga
Zanzibar mpya inayokabiliwa na matatizo ya kiuchumi, ajira na kupambana
na umaskini unaohitaji umoja, mshikamao na utulivu ili kuyashinda.
Naye Mkuu wa Jeshi la Polisi Nchini, Inspekta Jenerali, Saidi Mwema
alisema watawakamata na kuwafikisha mahakamani watakaohusika na vurugu
hizo na kwamba jeshi lake limejipanga kukabiliana na vurugu.
Habari-Tanzania Daima
| | | | | | | | | | | | . | | | | | | | | | | |
No comments:
Post a Comment