Wednesday, October 23, 2013

'Nyaisangah alikuwa baba bora wa familia yetu'


 Mjane wa Julius Nyaisangah, Leah.

Mke wa mtangazaji mkongwe nchini, Julius Nyaisangah, Leah amesema, mumewe alianza kusumbuliwa na ugonjwa wa Kisukari tangu mwaka 2009.

“Kama alikuwa nayo kabla hatujui lakini tuligundua kuwa mume wangu mpenzi ana sukari mwaka 2009 na baadaye ikagundulika pia alikuwa na shinikizo la damu, tangu hapo amekuwa akiteseka sana,” alieleza mama huyo akijitahidi kuzuia machozi.

Alisema, licha ya kuugua mumewe alikuwa hodari wa kufanya kazi na kuendelea na majukumu yake muda wote katika Kampuni ya Abood Media aliyokuwa akifanya kazi mpaka mauti yalipomkuta.

“Kwa kweli alijitahidi sana, alikuwa baba bora kwa familia yetu lakini Mungu amempenda zaidi. Namuombea makazi mema,” alisema.
 
Bi. Leah alisema, mumewe alikuwa akipatiwa matibabu katika hospitali mbalimbali mjini hapa na kuendelea na dawa lakini miezi mitatu iliyopita hali ilikuwa mbaya zaidi na alipumzika kwenda kazini kwa kipindi chote cha miezi mitatu.

“Lakini alipata nafuu na kurudi kazini, hadi wiki iliyopita alikuwa kazini kama kawaida ila sasa sukari ikapanda tena ghafla, halafu na presha nayo ikawa juu huku akiwa na malaria, ndipo akafariki,” alisema kwa uchungu.

Risasi

No comments:

Post a Comment