Wednesday, October 23, 2013

Anahitaji msaada wako


Mtoto Selemani Rajabu
 
KAZALIWA mwaka 1996, kapata mateso kwa takribani miaka 17 , anahitaji msaada. Mtoto huyo hawezi kutembea au kufanya shughuli yoyote kwa sababu kavimba miguu kama unavyoiona, ili atoke sehemu moja kwenda nyingine inabidi abebwe.
 
Uvimbe ulianza kidogo kidogo kwenye nyayo, kadri anavyokua ndivyo unavyozidi kuongezeka,

“Mateso ninayopata siwezi kusimulia na sijui nini hatma ya maisha yangu kwani naishi katika mazingira magumu kutokana na maumivu katika miguu yangu,” anasema kwa masikitiko.
 
Selemani ni mkazi wa kwa Butu eneo la Bomba Mbili kwa Chela kata ya Kivule, Wilaya ya Ilala mkoa wa Dar es Salaam ambako anaishi na mama yake mzazi.

"Tangu nikiwa mdogo niliambiwa sijawahi kutembea hadi nilivyofikia hapa ninateseka," anasema.

Selemani anasema kutokana na hali yake inambidi ajisaidie hapo hapo kwa kuwa hawezi kwenda chooni.

Hata anapotolewa nje kupata hewa inambidi abebwe na watu wawili kutokana na uzito wa uvimbe wa miguu yake.

Anatamani aende shule lakini hali aliyonayo haimruhusu na hivyo kumkosesha haki zake za msingi.

Selemani anawaomba wasamaria wema walioguswa na tatizo lake wamsaidie kwa hali na mali ili aweze kwenda India kufanyiwa upasuaji.

Anasema wazazi wake wamehangaika katika hospitali mbalimbali ikiwamo Hospitali ya Taifa ya Muhimbili bila mafanikio. Aidha, walipoenda hospitali ya CCBRT, waliambiwa kuwa tatizo hilo hawawezi kulihudumiwa na kutakiwa kurudi nyumbani.

“Natamani ningepata mfadhili akanisaidia nikatibiwe huko India maana huwa nasikia watu wakipelekwa kutibiwa angalau huu mguu unywee niweze kutembea kama wenzangu ninapata shida sana hilo tu ndiyo linanisumbua,” anasema.

Yeyote atakayeguswa na tatizo la mtoto huyu anaombwa awasiliane na baba yake, Rajab Yusuph kwa simu 0718355563 au Mhariri wa gazeti la Nipashe Jumapili 0715268581.

No comments:

Post a Comment