Friday, July 29, 2011

Wabunge watatu watimuliwa bungeni


Wabunge wa Chadema, kutoka kushoto, Mchungaji Peter Msigwa, Godbless Lema, na Tundu Lissu (wa kwanza kulia),wakiwa na Mbunge mwenzao, John Mnyika nje ya ukumbi wa Bunge mjini Dodoma baada ya Naibu Spika wa Bunge, Job Ndugai kuwafukuza bungeni wabunge watatu.


Wabunge watatu wa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), akiwemo Mnadhimu Mkuu wa Kambi ya Upinzani Bungeni, Tundu Lissu (Singida Mashariki) jana walifukuzwa bungeni.


Naibu Spika wa Bunge, Job Ndugai pia aliwatimu Mbunge wa Arusha Mjini, Godbless Lema na Mchungaji Peter Msigwa (Iringa Mjini).


Walifukuzwa kutokana na kile Naibu Spika wa Bunge, Job Ndugai alichoeleza kuwa ni kukiuka Kanuni za Bunge zinazowataka kutozungumza chochote ndani ya bunge bila idhini ya kiti cha Spika.

Mbunge mwingine wa Chadema, Ezekiah Wenje (Nyamagana) juzi alitimuliwa bungeni kwa sababu hiyo hiyo.


Lissu, Lema na Msigwa walipewa adhabu hiyo baada ya kubishana na
Ndugai bila utaratibu, Wenje alifukuzwa kwa sababu alitaka mwongozo wa kiti cha Spika Mwenyekiti wa Bunge akakataa.


Lissu, Msigwa na Lema walipinga kile walichokiita muda mrefu aliokuwa amepewa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu ( Sera, Uratibu na Bunge), William Lukuvi, kueleza kukiukwa kwa kanuni za Bunge.


Lukuvi aliomba kupewa mwongozo wa Naibu Spika mara baada ya Lema ambaye ni Waziri Kivuli wa Mambo ya Ndani ya Nchi, kusoma hotuba ya maoni ya kambi ya upinzani kuhusu wizara hiyo ambayo ilikuwa na shutuma nyingi
dhidi ya Serikali, hasa Jeshi la Polisi

"Mwongozo wa Spika, mwongozo wa Spika........Mheshimiwa Naibu Spika sasa......," alisikika sauti ya Lissu wakati Lukuvi akiendelea kuzungumza, Ndugai akasimama na kumuonya.


"Nimesema hairuhusiwi kuwasha mic (kinasa sauti) yako bila ruhusa yangu...waziri endelea...." alisema Ndugai.


Baada ya kauli hiyo, ndipo vipaza sauti ambavyo haikuwa rahisi kufahamu idadi yake viliwashwa na sauti kuanza kusikika zikimkosoa Ndugai kwamba anapendelea, kwa madai kuwa Lukuvi alipewa muda mrefu wa kuomba utaratibu
tofauti na msimamo wa awali aliokuwa ameutoa Naibu Spika huyo

"Mheshimiwa Naibu Spika, haiwezekani ..." ilisikika sauti ya Msigwa huku sauti nyingine kadha wa kadha zikisikika bila mpangilio hali iliyosababisha taharuki na kuathiri shughuli za Bunge.


Sauti hizo zilisababisha mzozo na kukosekana kwa utulivu na usikivu bungeni hivyo Ndugai ambaye pia ni Mbunge wa Kongwa (CCM) akaamua kutumia rungu lake kuamuru wabunge hao watoke ndani ya ukumbi wa Bunge.


"Nilishasema tangu asubuhi na nimewakumbusha kwamba hakuna Mbunge anayeruhusiwa kuwasha microphone (kinasa sauti) na kuzungumza bila idhini ya kiti, sasa naanza kutumia kanuni, nimewaona wabunge watatu, Mheshimiwa
Lissu, Mheshimiwa Mchungaji Msigwa na Mheshimiwa Lema, tokeni nje," aliamuru Ndugai na kuongeza:


"Tena nitafuatilia kuhakikisha kwamba mnaondolewa kabisa nje ya geti (lango kuu) la kuingilia bungeni, muondoke kabisa katika eneo hili."

Wabunge hao walitoka nje huku wakisindikizwa na askari (wapambe) wa Bunge hadi nje ya ukumbi na baadaye kuondolewa kabisa katika eneo hilo, hivyo kutokuwa na fursa hata ya kuzungumza na waandishi wa habari.


Kwa mujibu wa kanuni za Bunge, wabunge hao jana hawakuruhusiwa kurejea tena bungeni siku hiyo, badala yake watarejea leo kwa kuwa adhabu yao ni kukosa kikao kwa siku moja tu.

No comments:

Post a Comment